MASHADA INC

Thursday, August 16, 2012

YANGA SC WAENDA KIGALI JUMATANO KUWEKA KAMBI


MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Yanga SC Jumatano ijayo wataondoka Dar es Salaam kwenda Kigali, Rwanda kuweka kambi ya kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Habari za ndani kutoka Yanga zimesema kwamba maandalizi yote ya safari hiyo yamekwishakamilika na klabu itakuwa huko kwa takriban wiki mbili ikijifua sambamba na kucheza mechi za kirafiki dhidi ya timu tishio za huko.

Miongoni mwa timu zitakazocheza mechi za kirafiki na mabingwa hao wa Kombe la Kagame ni APR, Rayon, Atracao na Polisi, ambazo ndizo timu tishio nchini humo. Mapema jana, kocha wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintfiet alisema anataka mechi mbili kabla ya kutoka nje ya nchi kwenda kuweka kambi fupi ya kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.

Mtakatifu Tom alisema kwamba mechi dhidi ya timu ya hapa nyumbani na nyingine dhidi ya timu ya nje na baada ya hapo atakuwa tayari kwa safari ya nje nchi na Katibu wa Yanga, Celestine Mwesigwa alisema wanaweza kucheza na African Lyon ya Dar es Salaam na AFC Leopard ya Kenya. Akiwa anaingia mwezi wa pili tangu aanze kazi Yanga, tayari Tom amekwishaweka Kombe moja kwenye kabati la mataji la Yanga, ambalo ni la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame. Yanga ilitwaa Kombe la Kagame kwa mara ya pili mfululizo wiki mbili zilizopita, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Azam FC mabao 2-0, ambayo yalitiwa kimiani na Hamisi Kiiza ‘Diego Milito’ na Said Bahanuzi ‘Spider Man’.

Hiyo kwa ujumla ilikuwa mara ya tano mfululizo, Yanga inatwaa Kombe hilo, baada ya awali kuchukua mwaka jana, wakiifunga Simba katika fainali bao 1-0, Uwanja wa Taifa mfungaji Kenneth Asamoah ambaye ametemwa, ingawa siku hiyo Kiiza pia alifunga bao safi, ambalo refa alilikataa. Yanga ilichukua kwa mara ya kwanza Kombe hilo, mwaka 1975 ikiifunga tena Simba katika fainali, mabao 2-0 wafungaji Sunday Manara ‘Computer’ na Gibson Sembuli (sasa marehemu) Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Ikachukua tena mwaka 1993, Uwanja wa Nakivubo, Kampala, Uganda kwa kuifunga SC Villa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na Said Nassor Mwamba ‘Kizota’ (sasa marehemu) na Edibily Jonas Lunyamila. Ilichukua tena mwaka 1999, ikiifunga tena SC Villa, Uwanja wa Nakivubo, kwa penalti 5-3, kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 120, Yanga ikisawazisha bao kupitia kwa Lunyamila, baada ya Hassan Mubiru kutangulia kuifungia Villa, siku hiyo Manyika Peter akicheza penalti mbili za Waganda.

Aidha, kwa kutwaa Kombe hilo chini ya Mbelgiji huyo, Yanga imeendeleza rekodi yake ya kutwaa mataji ya michuano hiyo, chini ya makocha wa kigeni baada ya mwaka 1975 kuchukua chini ya Tambwe Leya aliyekuwa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kabla ya kuchukua uraia wa Tanzania, (sasa marehemu), 1993 chini ya Nzoyisaba Tauzany aliyekuwa raia wa Burundi kabla ya kuchukua uraia wa Tanzania, mwaka 1999 chini ya Raoul Shungu wa DRC na mwaka jana chini ya Mganda, Sam Timbe.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...